Open top menu
Jumamosi, 30 Novemba 2013
 ZANZIBAR HEROES NJIA PANDA CHALENJI, YAKUBALI KIPIGO CHA 3-1 KUTOKA KWA ETHIOPIA

PICHA KWA HISANI YA BIN ZUBEIRY BLOG

ZANZIBAR Heroes imejiweka njia panda kwenda au kutokwenda Robo Fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Chalenji baada ya kuchapwa mabao 3-1 na Ethiopia mchana wa leo, Uwanja wa Nyayo, Nairobi, Kenya.

Mabao yaliyoizamisha Zanzibar leo yalifungwa na nahodha, Fasika Asfan dakika ya tano, Salahadin Bargicho kwa penalti dakika ya 37 baada ya Manaye Fantu kuangushwa kwenye eneo la hatari wakati Yonathan Kebede alifunga la tatu dakika ya 83.

Bao la Zanzibar lilifungwa na kiungo mpya wa Simba SC, Awadh Juma Issa dakika ya 68 kwa kichwa akiunganisha krosi ya Seif Abdallah Karihe, ambaye alimlamba chenga beki wa kulia wa Ethiopia kwanza.

Zanzibar ilipata pigo mapema tu dakika ya 14, baada ya mchezaji wake tegemeo Suleiman Kassim ‘Selembe’ kuumia nyama za paja na kutoka nje, nafasi yake ikichukuliwa na Seif Abdallah Karihe. 
 
Kwa kipigo cha leo, Zanzibar inabaki na pointi zake tatu ilizovuna kwa kuifunga Sudan Kusini 2-1 katika mchezo wa ufunguzi na Ethiopia iliyoanza kwa sare ya bila kufungana na wenyeji Kenya, inakuwa na pointi nne.



Read more
SALAMU ZA TFF KWENYE HAFLA YA KUPOKEA KOMBE HALISI LA DUNIA TANZANIA

Mheshimiwa Rais, nianze kwa kukushukuru kwa heshima uliyoupatia mpira wa Tanzania kwa kukubali kuwa mgeni rasmi katika hafla yetu hii ya kupokea Kombe halisi la Dunia.

Hii ni mara ya tatu kwa Tanzania kupewa heshima hii na FIFA na washirika wake kampuni ya vinywaji ya Coca-Cola.

Coca-Cola ni washirika wetu wa karibu na wamekuwa wakidhamini mashindano ya kitaifa ya vijana tangu mwaka 2007, mashindano ambayo kwa kiasi kikubwa yamesaidia kuibua vipaji vingi ambapo baadhi yao wameweza kuchezea timu zetu za Taifa na klabu za Ligi Kuu na Daraja la Kwanza.

Tunawashukuru sana Coca-Cola na tunaahidi  kuendelea kuwapa ushirikiano katika jitihada zao za kuendeleza soka ya vijana.

Mheshimiwa Rais, tarehe 19 Novemba, 2009 wakati unapokea kombe hili hili hapa Tanzania ulitoa changamoto kadhaa kwa uongozi wa mpira wa Tanzania.

Ulitushauri tuimarishe uongozi na utendaji wetu kuanzia ngazi ya Taifa, Mikoa, Wilaya hadi klabu, ulitushauri tupate walimu wenye uzoefu wa kutosha kufundisha timu zetu za mpira na pia ulitushauri tuwekeze katika kuibua na kuendeleza vipaji vya wachezaji toka wakiwa na umri mdogo.

Mheshimiwa Rais ushauri wako kwetu tuliuzingatia na tulifanya jitihada za kuufanyia kazi. Hali ya utulivu katika uendeshaji mpira wetu imeimarishwa na pale palipoonyesha dalili za migogoro tulikemea na ikibidi tulichukua hatua madhubuti kutatua migogoro.

Tumefanya kozi mbalimbali za kuwaendeleza walimu wetu wa mpira, waamuzi, madaktari na viongozi wetu wa ngazi mbalimbali na matokeo yake yanaonekana katika kuinuka kwa viwango vyao vya ufundishaji na utoaji uamuzi uwanjani.

Mheshimiwa Rais kama ulivyotuelekeza mwaka 2009 maendeleo ya soka ya vijana ndio ufunguo wa maendeleo ya mpira kwa Taifa letu. Uongozi mpya wa TFF ulioingia madarakani alfajiri ya tarehe 28, Oktoba 2013 tayari unalifanyia kazi jambo hili kwa umakini mkubwa.

Uongozi wetu umeamua kuwa ufunguo wa mpango endelevu wa soka ya vijana utakuwa ni Tanzania kuwa mwenyeji wa fainali za Afrika za vijana chini ya umri wa miaka 17 mwaka 2019.

Fainali hizi uhusisha mataifa manane yanayogawanywa katika makundi mawili ya awali akiwemo mwenyeji ambaye anaingia moja kwa moja kwenye hatua ya makundi ya fainali hizi. Aidha timu mbili zinazoongoza makundi haya mawili moja kwa moja huwa zinacheza fainali za dunia za vijana chini ya umri wa miaka 17.

Fainali hizi ndizo ziliwaibua akina Luis Figo, Ronaldino, Nwankwo Kanu, Michael Essien, Nii Lamptey, Celestine Babayaro na wengine kadhaa.

Ili tupate timu nzuri ya vijana umri chini ya miaka 17 mwaka 2019 itabidi mwaka kesho 2014 tufanye mashindano ya kitaifa ya vijana chini ya umri wa chini wa miaka 12 ili tupate kikosi cha kwanza cha Taifa U-12, kikosi ambacho kitakuwa pamoja kuelekea 2019.

Katika kuboresha kikosi hiki mwaka 2015 tutafanya mashindano ya kitaifa ya umri chini ya miaka 13, 2016 yatakuwa ya umri chini ya miaka 14, 2017 yatakuwa ya umri chini ya miaka 15 na 2018 yatakuwa ya umri chini ya miaka 16 na ambayo yatatupatia kikosi cha mwisho cha kuingia nacho fainali za vijana mwaka 2019.

Tunaamini timu nzuri za Taifa U-17 ya mwaka 2019 itatuzalishia kikosi imara kitakachoshiriki Olimpiki za 2020, kucheza CHAN na AFCON zitakazofuata na hatimae kufaulu fainali za dunia 2026 ambayo ni miaka kumi na tatu kuanzia sasa.

Ninashukuru tarehe 21 Novemba 2013, Shirikisho la mpira barani Afrika (CAF) liliniteua kuwa Mjumbe wa Kamati ya Maandalizi ya michuano ya Afrika umri chini ya miaka 17 (CAF U-17 Organizing Committee), tunaamini kuwepo kwangu katika kamati hii muhimu ya CAF kutasaidia Tanzania ipate wenyeji huu mwaka 2019.

Mheshimiwa Rais kwa mujibu wa kanuni za CAF nchi inayoomba uenyeji wa fainali za michuano ya Afrika haina budi ionyeshe barua ya kuungwa mkono na nchi yake(Letter of support from Government).

Wiki ijayo tutawasilisha barua kwenye Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ya kuomba kuungwa mkono na Serikali katika azma yetu hii, tunaomba Serikali ituunge mkono katika jambo hili.

Mheshimiwa Rais nimalizie kwa kukushukuru tena kwa uwepo wako katika shughuli hii muhimu, ninaishukuru Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kwa ushirikiano wanaotupa katika shughuli zetu za kila siku, FIFA nawashukuru sana kwa kutuwezesha kuwa moja ya nchi 88 duniani zilizopokea kombe hili, Coca-Cola asanteni sana tuzidi kuwa karibu.


Watanzania wenzangu ninaomba tuje kwa wingi kesho Jumamosi kutembelea Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kuliona Kombe hili na kupiga nalo picha. Imani yangu ni kuwa ipo siku Kapteni wa Timu yetu ya Taifa atamkabidhi Rais wa Tanzania kombe hili.
Read more
KOCHA WA CAMEROON ASAINI MIAKA MWILI AZAM

Kocha mpya wa Azam FC. Joseph Marius Omog (katikati) akizungumza na waandishi wa habari mara tu baada ya kusaini mkataba wa kuifundisha timu hiyo.

KLABU ya Azam inapenda kuufahamisha umma hususan wapenzi wa mpira wa miguu kuwa imeingia mkataba na kocha Joseph Marius Omog raia wa Cameroon kwa kipindi cha miaka miwili (2) kuanzia leo.

Kocha Omog ni bingwa kwani anakuja kuifundisha Azam akiwa ametoka kuiongoza klabu ya A.C Leopards ya Jamhuri ya Kongo (Brazaville) kutwaa ubingwa wa ligi ya nchi hiyo kwa misimu miwili mfululizo (2012 na 2013).

Timu hii ilikuwa haijatwaa ubingwa wa ligi kwa zaidi ya miaka 30. Kwa mwaka huu wametwaa ubingwa wakiwaacha wapinzani wao, Diables Noirs kwa pengo la pointi kumi (10) wakikusanya pointi 87 katika ligi yenye timu 18.

Pia ni mwaka jana tu (2012) aliiwezesha A.C Leopards kunyakua ubingwa wa Kombe la Shirikisho la Afrika kwa kuzipiga kumbo timu ngumu na zenye uzoefu mkubwa kama vile Mas de Fes ya Morocco, Heartlands ya Nigeria na Sfaxien ya Tunisia.

Mafanikio hayo ya kutwaa ubingwa wa Afrika yalifikiwa baada ya miaka 38 tangu klabu ya Jamhuri yas Kongo ifanye hivyo, na kumfanya kocha Omog kuwa moja ya makocha wa kupigiwa mfano barani Afrika.

Kadhalika mwaka huu 2013, A.C Leopards chini ya ukufunzi wa Omog ilitinga hatua ya makundi ya Ligi ya mabnigwa Afrika na kupangwa katika kundi moja na timu mbili zilizocheza fainali; Al Ahly ya Misiri (bingwa) na Orlando Pirates ya Afrika Kusini.

Yote hayo ameyafanya akitumia asilimia kubwa ya wachezaji wa ndani ya Kongo huku akiwainua kutoka katika hali ya kuonekana wachezaji wa wastani hadi kuwa tishio na kuhofiwa kote barani Afrika.

Azam Football Club inamuona kocha Omog kuwa anakidhi vigezo vya kuendana na dira ya klabu ambayo ni kukuza na kuwaendeleza wachezaji na kushindana kwa kiwango cha juu kwa lengo la kuwa mabingwa katika mashindano mabalimbali ambayo timu inashiriki.

Uongozi wa Azam FC utampatia ushirikiano wa kutosha ili kufanikisha malengo na mipango thabiti ya klabu.

Maelezo Binafsi
Kocha Omog ni mchezaji wa zamani wa timu ya Dragon Yaounde Cameroon. Alipata mafunzo ya ualimu wa michezo na elimu ya viungo (Sports and physical education) kutoka chuo cha vijana na michezo (Higher Institute of Youth and Sports, INJS Yaounde).

Baadaye alipata fursa ya kujiendeleza nchini Ujerumani ambako mwaka 1987 alitunukiwa stashahada ya ukufunzi wa mpira wa miguu na leseni B ya ukocha kwa viwango vya Shirikisho la mpira wa miguu barani Ulaya, UEFA.

Aliporejea nyumbani kwao Cameroon Joseph Marius Omog, alifundisha kabumbu katika klabu mbalimbali, zikiwemo; Fovu of Baham na Aigle of Menoua na kufanikiwa kufuzu kwa fainali za kombe la Cameroon. Mwaka 2001 aliteuliwa kocha msaidizi wa timu ya taifa ya Cameroon, Indomitable Lions chini ya kocha raia wa Ujerumani Winfried Schafer.


Omog amewahi pia kufundisha timu ya taifa ya Cameroon iliyoundwa na wachezaji wa ndani ijulikanayo kama Intermediate Lions hadi mwaka 2010 na baada ya hapo akelekea Kongo kuionoa A.C Leopards kwa mafanikio makubwa na hasa kutwaa ubingwa wa kombe la Shirikisho wakiifunga Djoliba ya Mali kwa ushindi wa jumla wa magoli 4-3 katika michezo miwili ya fainali.
Read more
UMEWAHI KUIONA HII PICHA? RAGE AKIMALIZA BIASHARA YA OKWI

NDANI ya Simba sasa kumewaka moto kutokana na Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo pamoja na wanachama ambao hawana imani na Mwenyekiti wao, Ismail Aden Rage hali iliyopeleka kutaka kumpindua mara mbili ndani ya mwaka huu.

Moja katika madai ambayo yanamtia matatani Rage ni kuuzwa kwa mshambuliaji wao, Emmanuel Okwi kwa Etoile du Sahel ya Tunisia kwani hadi sasa fedha za kuuzwa mwanandinga huyo imekuwa ni kitendawili.

Pichani Rage anaonekana akipiga picha akipena mikono na mmoja wa viongozi wa Etoile du Sahel mara baada ya kumalizana biashara ya kuumza mshambuliaji huyo.



  
Read more
KOCHA WA AZAM ATUA LEO KUANZA KAZI

Joseph Marius Omog baada ya kuwasili uwanja wa ndege wa JNIA kwa kazi ya kuifundisha Azam FC

KOCHA mpya wa timu ya Azam FC, Joseph Marius Omog amewasilia leo asubuhi tayari kwa kuifundisha timu hiyo katika mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya Kombe la Shirikisho.

Kocha huyo raia wa Cameroon ambaye alikuwa akiifundisha timu ya AC Leopards ya Congo Brazzavile amewasili leo asubuhi akitokea kwao tayari kabisa kwa kuanza kibarua chake.

Kocha huyo mwenye mafanikio makubwa barani Afrika amekuja kuchukua nafasi ya Stewart Hall ambaye ametupiwa virago mara tu baada ya kumalizika kwa mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo.
Read more
Ijumaa, 29 Novemba 2013
FIFA WAFUNGUKA BAADA YA UWANJA WA KOMBE LA DUNIA KUPOROMOKA BRAZIL

SHIRIKISHO la Kimataifa la Mpira wa Miguu (Fifa) imesema halina mpango wa kuhamisha michuano ya Fainali ya Kombe la Dunia 2014 kutoka nchini Brazil ingawa nchi hiyo imepata changamoto katika maandalizi ya michuano hiyo.

Wafanyakazi wawili walipoteza maisha baada ya kuangukiwa na nguzo ambazo ziliharibu uwanja wa Corithians ulio mjini Sao Paulo.

Timu ya taifa ya Brazil inatarajiwa kucheza mechi ya ufunguzi ya Kombe la dunia katika uwanja huo wenye uwezo wa kuwa na watazamaji 65,000.

Vyanzo vya habari vya juu ndani ya Shirikisho hilo vimeendelea kusisitiza kuwa hakuna mbadala kutokana na kutokea kwa ajali hiyo.

Brazil ilikiri kuwa inafanya jitihada za kumaliza ujenzi wa viwanja 12 kwa ajili ya michuano hiyo, sita kati ya hivyo ipo tayari kwa ajili ya michuano ya kombe la shirikisho.

Ajali iliyotokea siku ya Jumatano ni ya tatu kusababisha kifo katika viwanja vitakavyopigiwa kipute cha kombe la dunia. Wafanyakazi wengine wawili walipoteza maisha kipindi cha miaka miwili iliyopita.

Uchunguzi umeanza hii leo kubaini chanzo cha ajali mjini Sao Paulo.
Read more
Alhamisi, 28 Novemba 2013
MAN UNITED YAWAPIGA WAJERUMANI 5-0, MAN CITY, MADRID ZAUA, BAYERN YAVUNJA REKODI YA BARCELONA

MANCHESTER United imefanya mauaji makubwa ugenini, baada ya kuitandika Bayer Leverkursen mabao 5-0 nchini Ujerumani katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa ya Ulaya.  

Mabao ya United yamefungwa na Valencia dakika ya 22, Spahic aliyejifunga dakika ya 30, Evans dakika ya 65, Smalling dakika ya 77 na Nani dakika 88. Wayne Rooney ndiye alikuwa nyota wa mchezo kutoka na kupika mabao manne katika ushindi huo ambao haukutarajiwa.  

Katika mchezo mwingine, winga Gareth Bale amewaongoza wachezaji 10 wa Real Madrid kuibuka na ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya timu ya Roberto Mancini, Galatasaray, akifunga bao tamu la mpira wa adhabu kipindi cha kwanza.

Huku Cristiano Ronaldo akiushuhudia mchezo huo kutoka jukwaa la VIP Uwanja wa Bernabeu, hakuna aliyeweza kumzuia Bale kufunga kwa mpira wa adhabu dakika ya 37.

Mabao mengine ya Real yalifungwa na Arbeloa dakika ya 51, Di Maria dakika ya 63 Isco dakika ya 80, wakati bao pekee la Galatasaray lilifungwa na Bulut dakika ya 38. 

Manchester City nao wameifumua mabao 4-2 Viktoria Plzen Uwanja wa Etihad katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya. Mabao ya City yamefungwa na Aguero kwa penalti dakika ya 33, Nasri dkika ya 65, Negredo dakika ya 79 na Dzeko dakika ya 90, wakati mabao ya Viktoria Plzen yamefungwa na Horava dakika ya 43 na Tecl dakika ya 69. 

Jana usiku mabingwa watetezi, Bayern Munich wameendeleza ubabe katika Ligi ya Mabingwa baada ya kuicharaza mabao 3-1 CSKA Moscow Uwanja wa Khimki Arena katika mchezo wa Kundi D.

Mabao ya Bayern usiku huu yamefungwa na Arjen Robben, Mario Gotze na Thomas Muller kwa penalti. Huo unakuwa ushindi wa 10 mfululizo kwa Bayern na hivyo kuvunja rekodi ya mwaka 2002 ya Barcelona katika michuano hiyo.
  Winga wa Manchester United, Luis Nani akifunga bao la tano
   Wachezaji wa Manchester United wakishangilia nao la Johny Evans
   Kiungo wa Real Madrid, Sergio Ramos akitolewa kwa kadi nyekundu
   Mshambuliaji wa Galatasaray, Bulut akifunga bao pekee kwa timu yao
    Mshambuliaji wa Manchester City, Aguero akishangilia bao 








Read more
Jumatano, 27 Novemba 2013
ZANZIBAR MWENDO MDUNDO CHALENJI, YAICHAPA SUDAN KUSINI 2-1

ZANZIBAR imeanza vyema michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki na Kati, CECAFA Chalenji baada ya kuifuga mabao 2-1 Sudan Kusini katika mchezo wa ufunguzi wa Kundi A, Uwanja wa Nyayo, Nairobi, Kenya.

Mabao ya Zanzibar Heroes leo yalifungwa na kiungo wa Coastal Union ya Tanga, Suleiman Kassim ‘Selembe’ dakika ya saba baada ya kuipangua ngome ya Sudan Kusini na kufumua shuti lililomshinda kipa Juma Jinaro na Adeyoum Saleh Ahmed dakika ya 67.

Bao la Sudan Kusini lilifungwa na Fabiano Lako dakika ya 73, zikiwa ni dakika tano aiingie kuchukua nafasi ya Francis Khamis.

Zanzibar ingeweza kuondoka na ushindi mnene leo kama washambuliaji wake, Khamis Mcha ‘Vialli’ na Ally Badru wangetumia vyema nafasi nzuri walizopata.

Nafasi nzuri zaidi ambayo Zanzibar walipata ilikuwa dakika ya 43 baada ya Badru kumlamba chenga kipa, lakini Khamis Mcha alipopiga mpira ukagonga mwamba na kipa akaudaka.

Zanzibar; Abdallah Rashid, Salum Khamis/Ally Khan dk78, Waziri Salum, Shaffi Hassan, Mohamed Fakhi, Sabri Ali, Masoud Ali, Suleiman Kassim, Awadh Juma na Khamis Mcha/Amour Omar dk44/Adeyoum Saleh dk62.


Sudan Kusini; Juma Jinaro, Atar Thomas, Philip Delfino, Edomon Amadeo, Richard Justin, Wiiam Offiri, Jimmy Erasto, Thomas Jacob, Godfrey Peter, Francis Khamis/Fabiano Lako dk68 na James Joseph.
Read more
ARSENAL YAUA 2-0, CHELSEA YAKALISHWA, BARCA NAYO CHALIIII, BALOTELLI AING'ARISHA AC MILAN

MABAO mawili ya kiungo Jack Wilshere leo yameipa ushindi wa 2-0 Arsenal dhidi ya Marseille ya Ufaransa katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya usiku huu Uwanja wa Emirates.

Ilimchukua sekunde 29 tangu kuanza kwa mchezo huo kiungo huyowa England kufunga bao la kwanza akimtungua kipa hodari, Steve Mandanda na akfunga tena bao la pili dakika ya 65. 

Nayo Barcelona jana ilionja joto ya jiwe baada ya kukubali kichapo cha mabao 2-1 kutoka kwa Ajex katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya mjini Amsterdam. Pamoja na ushindi huo, Ajax ilimaliza pungufu ya mchezaji mmoja baada ya Veltman kutolewa nje kwa kadi nyekundu dakika ya 48.

Mabao ya Ajax yalifungwa na Serero dakika ya 18 na Hoesen dakika ya 41 kabla ya Xavi kuifungia Barca bao la kufutia machozi kwa penalti dakika ya 49.
 

Katika mchezo mwingine, Chelsea imefungwa bao 1-0 na FC Basle, bao pekee la Mohamed Salah. Mabao ya Kaka dakika ya 12, Zapata dakika ya 49 na Balotelli dakika ya 59 yameipa AC Milan ushindi wa 3-0 dhidi ya Celtic nchini Scotland katika mchezo mwingine wa michuano hiyo. 






Read more
Jumatatu, 25 Novemba 2013
CHUJI, CANNAVARO, YONDANI, MSUVA,TEGETE WAJIFUNGA YANGA, SASA KUKIPIGA HADI 2016

WACHEZAJI watano wa timu ya Yanga wameongeza mikataba ya muda mrefu ambapo sasa wataendelea kuitumikia klabu yenye maskani yake mitaa ya Twiga/Jangwani mpaka mwaka 2016, hili limefanywa na uongozi kwa mapendekezo ya benchi la ufundi.

Wachezaji ambao mpaka sasa wameshaongeza mikataba ya kuitumikia klabu ya Yanga ni walinzi Kelvin Yondani (2014-2016), Nadir Haroub "Cannavaro" (2014-2016), kiungo Athuman Idd ‘Chuji’ (2014-2016), mshambuliaji Saimon Msuva (2014-2016) na Jerson Tegete (2014-2016).

Mwenyekiti wa kamati ya usajili wa klabu ya Yanga, Abdallah Bin Kleb amesema hao ni baadhi tu ya wachezaji ambao wameshamaliza taratibu zote na kusaini mikataba mipya itakayowafanya waitumikie Yanga mpaka mwaka 2016.

"Tupo katika mazungumzo ya mwisho na wachezaji wetu wengine, mazungumzo yanaendelea vizuri na tunaamini muda si mrefu nao tutakua tumeshamalizana nao ili waweze kuendelea kuitumika Yanga tena kwa muda mrefu "alisema Bin Kleb.


Wakati huo huo kikosi cha Yanga leo kimeanza mazoezi asubuhi katika uwanja wa Bora - Mabatini Kijitonyama kujiandaa na mchezo wa hisani dhidi ya Simba SC Disemba 14, 2013, mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom pamoja na mashindano ya kimataifa ya Ligi ya Klabu Bingwa Afrika.
Read more