RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya
Mrisho Kikwete ametoa changamoto kwa uongozi mpya wa Shirikisho la Mpira wa
Miguu Tanzania (TFF) kusukuma mbele zaidi gurudumu la maendeleo ya mchezo huo
nchini.
Ametoa changamoto hiyo katika barua yake kwa Rais
mstaafu wa TFF, Leodegar Tenga na kumtaka asichoke kutoa ushauri na uzoefu wake
kila utakapohitajika katika shughuli mbalimbali zinazohusu maendeleo ya mpira
wa miguu Tanzania.
Rais Kikwete ametoa changamoto hiyo wakati akijibu
barua ya Tenga iliyokuwa ikimuarifu kuhusu kumaliza kipindi chao cha uongozi,
na kumshukuru yeye binafsi (Rais Kikwete) na Serikali anayoiongoza kwa mchango
waliotoa katika kuendeleza mpira wa miguu nchini.
“Pongezi zako zimetupa moyo na ari ya kuongeza
maradufu juhudi zetu za kuboresha kiwango cha ubora wa mchezo wa mpira wa miguu
nchini.
“Kwa niaba ya Serikali napenda kuchukua nafasi hii
kutoa pongezi za dhati kwako wewe na uongozi wote uliopita wa TFF kwa mchango
wenu muhimu mlioutoa wa kuendeleza mpira wa miguu nchini.
“Mafanikio ya kutia moyo yamepatikana chini ya
uongozi wako,” amesema Rais Kikwete katika barua yake hiyo na kumtakia kila la
heri Tenga katika shughuli zake.
Hata hivyo, ameongeza kuwa Tanzania bado haijafika
pale ambapo inapataka, lakini dalili njema zimeanza kuonekana, hivyo
kinachotakiwa sasa ni uongozi mpya kusukuma mbele zaidi gurudumu la kuendeleza
mpira wa miguu nchini.
Tenga ambaye hivi sasa ni mjumbe wa Kamati ya
Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) na Mwenyekiti wa Baraza la
Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) aliiongoza TFF kwa
vipindi viwili kuanzia Desemba 2004 hadi Oktoba 2013.
0 comments