MSANII wa muziki wa kizazi kipya 'Bongo Fleva' Amin
na kundi la Sanaa la Makhirikhiri wa bongo ni miongoni mwa burudani zitakazosindikiza
onyesho maalumu la 'Usiku wa Banza Stone’
la bendi ya Extra Bongo 'Next Level' Wazee wa Kizigo.
Onyesho hilo maalum kwa ajili ya kumtambulisha
mtunzi na mwimbaji wake Ramadhani Masanja 'Le General Banza Stone' anayerejea
upya jukwanii Jumamosi hii ndani ya Meeda Club Sinza jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa msemaji wa bendi hiyo Juma Kasesa,
maandalizi ya onyesho hilo yamekamilika na tayari Banza ameanza mazoezi makali
ya kufua sauti yake tayari kuwapa burudani mashabiki na wapenzi wa muziki wa
dansi waliokuwa wame-mis sauti na tungo zake.
Kwa muda wa miezi mitatu Banza alikuwa yu mgonjwa
hali iliyomsababishia kushindwa kupanda jukwaani kabla ya mwishoni mwa mwaka
jana kujikongoja na kushiriki kwenye ziara ya 'Mafahari Watatu' katika Mikoa ya
Kanda ya Ziwa akiwa na bendi hiyo lakini
akalazimika kupewa mapumziko ili aweze kufanya mazoezi na kula kwa mpangilio
ili aweze kuimarisha afya yake.
Alisema, Amin na Makhirikhiri wa Bongo ni
sehemu tu ya burudani zitakazopamba
'usiku wa Banza Stone' kwani kutakuwa na vikundi vingine vya sanaa
vitakavyonogesha onyesho ambapo mara baada ya onyesho hilo wataendelea
kumtambulisha Banza katika kumbi mbalimbali za burudani jijini Dar es Salaam
kabla ya kufanya ziara nyingine katika baadhi ya Mikoa.
0 comments