Open top menu
Alhamisi, 21 Novemba 2013

Na Erasto Stanslaus               
KIM Poulsen, Kocha mkuu wa Taifa Stars aliyejijengea umaarufu kwa kutengeneza kikosi kamambe cha ushindi, sasa anasumbuliwa na Matokeo Makubwa Sasa.

Mipango yake ni ya dharura. Kocha huyo aliyekuwa anategemea timu za vijana za Ngorongoro Heroes (U-20) na Serengeti Boys (U-17) kama vitalu vya kupata wachezaji wa baadaye wa Stars amebadilika ghafla na kubaki akitegemea wakongwe.

Mfano, katika uteuzi wa Stars hivi karibuni Kim aliamua kutengeneza kundi jipya lisilo na daraja akaliita Future Young Stars yaani Nyota wa Stars ya Baadaye.

Kundi hilo la Future Young Stars ni la akina Aishi Manula, Hussein Shariff, Ivo Mapunda, David Luhende, Hassan Mwasapili, Himid Mao, Issa Rashid, Ismail Gambo, John Kabanda, Kessy Khamis, Michael Pius, Miraji Adam, Mohamed Hussein, Said Moradi na Waziri Salum.

Wengine ni Amri Kiemba, Farid Mussa, Haruni Chanongo, Hassan Dilunga, Jonas Mkude, Khamis Mcha, Ramadhan Singano, Simon Msuva, William Lucian, Elias Maguli, Hussein Javu, Joseph Kimwaga, Juma Liuzio, Mwagane Yeya na Paul Nonga.

Lakini aliowaita kuunda Taifa Stars ni Ally Mustafa, Mwadini Ali, Aggrey Morris, Kelvin Yondani, Shomari Kapombe, Nadir Haroub, Erasto Nyoni, Vincent Barnabas, Salum Abubakar, Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Athuman Idd, Mrisho Ngassa, Thomas Ulimwengu, Mbwana Samata na John Bocco.

Wachezaji 16 kutoka Future Young Taifa Stars wameungana na 16 wa Taifa Stars kuunda timu kamili ambayo ilicheza mchezo wa kirafiki dhidi ya Zimbabwe na kutoka suluhu. Stars ilielemewa sana hasa kipindi cha pili na mashabiki wa Stars hawakuridhishwa na kiwango cha kikosi hicho hivyo walipandwa na hasira na kuanza kumzomea Kim mara baada ya mchezo kumalizika.

Tujiulize, Ivo Mapunda aliyeichezea Stars akaachwa kwa madai kiwango kimeshuka nafasi yake ikatwaliwa na Juma Kaseja bado leo tunaambiwa ni Future Young Taifa Stars?

Umri wa Amri Kiemba ambaye leo anaitwa matumaini ya baadaye ni mkubwa kuliko Frank Domayo au Aboubakar Salum ambao ni matumaini ya sasa. Nani alipaswa kuwa matumaini ya  baadaye kati ya wachezaji hao?

Inawezekanaje Said Morad na Hussein Javu wawe matumaini ya baadaye wakati Thomas Ulimwengu na Shomari Kapombe ni mategemeo ya sasa?

Hapa ni wazi kuwa Kim ama amefikia ukomo wa ujuzi wake au anataka Matokeo Makubwa Sasa. Anataka timu ya kushinda michezo sasa na siyo hicho kiitwacho Future Young Taifa Stars.

Kwa mfumo anaoutumia Kim kuwategemea vijeba zaidi kuliko vijana ni ngumu kupata mafanikio yenye mwendelezo. Inawezekana timu ikaonekana ‘bora’ sasa lakini ikapotea kabisa katika ramani ya soka.

Kama kweli Kim angekuwa na nia ya kweli ya kuiboresha Stars baada ya kushindwa kupata nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia mwakani na zile za Afrika, ulikuwa muda muafaka wa kutengeneza kikosi cha baadaye cha Stars kwa kuwatumia wachezaji vijana wa Serengeti na Ngorongoro.

Hii inaonesha kuwa hakuna mipango ya kufanya vizuri kwa miaka ya baadaye kwani mfumo huu unawapoteza wachezaji vijana na kuwabeba vijeba ambao safari yao kisoka imefikia tamati.


MAKALA IMETOKA GAZETI LA MAWIO
Tagged
Different Themes
Written by Templateify

Aenean quis feugiat elit. Quisque ultricies sollicitudin ante ut venenatis. Nulla dapibus placerat faucibus. Aenean quis leo non neque ultrices scelerisque. Nullam nec vulputate velit. Etiam fermentum turpis at magna tristique interdum.

0 comments