Open top menu
Jumanne, 19 Novemba 2013

TIMU ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars leo imeshindwa kuutumia vizuri uwanja wa nyumbani baada ya kulazimishwa suluhu na Zimbabwe jioni hii katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Hata hivyo, Zimbabwe wangeondoka na sherehe Uwanja wa Taifa, kama si Refa Ronnie Kalema aliyesaidiwa na Samuel Kayondo na Lee Okelo wote kutoka Uganda kuwakatalia bao zuri lililofungwa na Sithole Simba dakika ya 90.

Kwa ujumla, Tanzania haikuwafurahisha mashabiki wake leo pamoja na kuwa na kikosi chake kamili, wakiwemo washambuliaji tegemeo Mbwana Samatta, Thomas Ulimwengu wanaocheza TP Mazembe ya DRC, kiungo Mwinyi Kazimoto anayechezea Al Markhiya ya Qatar na beki Shomari Kapombe anayechezea AS Cannesd ya Ufaransa.
Stars iliuanza vyema mchezo huo, safu ya kiungo ikiundwa na chipukizi Hassan Dilunga aliyecheza pamoja na Frank Domayo na Mwinyi Kazimoto.

Viungo hao waliweza kuwachezesha vizuri washambuliaji watatu wa Stars, Mrisho Ngassa, Thomas Ulimwengu na Mbwana Samatta, lakini wakashindwa kutumia nafasi hizo vizuri kipindi cha kwanza.
Zimbabwe walizinduka baada ya dakika 10 na kucheza vizuri, wakitengeneza nafasi pia ambazo walishindwa kuzitumia.

Safu ya kiungo ya Stars ilikufa ndani ya dakika 30 na Zimbabwe wakaanza kutawala mchezo. Kipindi cha pili, Kim alifanya mabadiliko ya viungo akiwaingiza Amri Kiemba na Salum Abubakar ‘Sure Boy’ kuchukua nafasi za Kazimoto na Dilunga na kidogo Stars ilianza kutawala sehemu ya katikati ya Uwanja, lakini iliishia kukosa mabao ya wazi.

Nafasi ambayo Stars wataijutia zaidi ni ya dakika ya 75, kufuatia Kapombe kutia krosi nzuri baada tya kupokea pasi ya Sure Boy, lakini Ulimwengu akazidiwa na kipa Tapiwa Kapini aliyedaka mpira miguuni mwake.
Kipa Ivo Mapunda alifanya kazi nzuri kwa kuokoa michomo mitatu ya hatari hali ambayo ilifanya ashangiliwe baada ya mechi.
Mashabiki walimzomea kocha Mdenmark Kim Poulsen baada ya mechi wakimuambia timu imemshinda na kumtaka aondoke.


Kikosi cha Tanzania kilikuwa; Ivo Mapunda, Shomari Kapombe, Erasto Nyoni/Himid Mao dk56, Aggrey Morris, Kevin Yondan, Frank Domayo, Hassan Dilunga/Salum Abubakar dk51, Mwinyi Kazimoto/Amri Kiemba dk51, Thomas Ulimwengu, Mbwana Samatta na Mrisho Ngassa/Farid Mussa dk80.
Tagged
Different Themes
Written by Templateify

Aenean quis feugiat elit. Quisque ultricies sollicitudin ante ut venenatis. Nulla dapibus placerat faucibus. Aenean quis leo non neque ultrices scelerisque. Nullam nec vulputate velit. Etiam fermentum turpis at magna tristique interdum.

0 comments