Wallace Karia
WANAMICHEZO wawili walioomba kuwania uongozi kwenye
uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) utakaofanyika Oktoba 27
mwaka huu wamewekewa pingamizi.
Waliopingwa ni Wallace John Karia anayeomba
kupitishwa kuwania urais na Vedastus Kalwizira Lufano anayewania ujumbe wa
Kamati ya Utendaji kupitia Kanda Namba Mbili ambayo ni mikoa ya Mara na Mwanza.
Anyempinga Karia ni Shamsi Rashid Kazumari wa Dar es Salaam wakati Lufano
anapingwa wa Samwel Nyalla wa Mwanza.
Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura, alisema pamoja
na mambo mengine, Kazumari anampinga Karia kwa madai kuwa akiwa Mwenyekiti wa
Kamati ya Ligi, aliwashawishi wajumbe wenzake kuingia mkataba na Azam Tv wakati
akijua kamati hiyo ni ya muda, hivyo haina nguvu za kisheria kusaini mkataba
huo.
Wambura alisema Nyalla ambaye pia ni mmoja wa
wanamichezo waliojitokeza kuwania ujumbe kupitia Kanda hiyo anampinga Lufano
kwa madai hana uzoefu wa miaka mitano katika uongozi wa mpira wa miguu.
Kamati ya Uchaguzi ya TFF chini ya Mwenyekiti wake
Hamidu Mbezeleni itakutana kesho (Agosti 28 mwaka huu) saa 4 kamili asubuhi
kusikiliza pingamizi hizo ambapo wawekaji pingamizi na waliopingwa wanatakiwa
kufika wenyewe ndani ya muda kwa vile uwakilishi hautakiwi.
0 comments