Kikosi cha Yanga
MICHUANO ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL)
inaingia raundi ya pili leo kwa timu zote 14 kuwa katika viwanja tofauti.
Lakini pambano linaloonekana kuvuta hisia za watu ni
lile kati ya timu ya Yanga dhidi ya Coastal Union ya Tanga.
Mechi hiyo inapigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es
Salaam kuanzia saa 10.30 jioni, ambapo kiingilio kwa mujibu wa Shirikisho la
Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ni sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh.
20,000. Mwamuzi aliyepangwa kuchezesha mchezo huo ni Martin Saanya kutoka
Morogoro, wakati Kamishna ni Omari Walii wa Arusha.
Mechi nyingine itakuwa katika Uwanja wa Manungu,
Turiani mkoani Morogoro, ambapo Mtibwa Sugar inaikaribisha Kagera Sugar, wakati
katika Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora, wenyeji Rhino Rangers Rangers
watakuwa wakiialika Azam FC ya Dar es Salaam.
Vumbi lingine litatimka kwenye Uwanja wa Mabatini
ulioko Mlandizi, Pwani, wakati maafande wa JKT Ruvu watakapokwaruzana na wenzao
wa Tanzania Prisons kutoka Mbeya. Mbeya City na Ruvu Shooting zitacheza kwenye
Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.
Jiji la Tanga litakuwa mwenyeji wa mechi kati ya
Mgambo Shooting na Ashanti United itakayochezwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani.
Oljoro JKT itakuwa mwenyeji wa mabingwa wa zamani, Simba kwenye Uwanja wa
Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha.
0 comments