Open top menu
Alhamisi, 22 Agosti 2013



Na Erasto Stanslaus
SAKATA la usajili  wa kiungo mshambuliaji wa timu ya soka ya taifa, Mrisho Ngassa linaonyesha kwamba kanuni za mikataba na usajili wachezaji wa mkopo zinatakiwa kuongezewa makali.
Simba iliposoma kanuni hizo iligundua upenyo hivyo baada ya kumchukua Ngassa kwa mkopo akitokea Azam FC iliamua kuingia mkataba mpya juu kwa juu.
Yanga nao baada ya kujua wamewahi kuitibulia Simba kwa usajili wa Kelvin Yondani na Mbuyu Twite bila kuadhibiwa, ilijitosa kukamilisha usajili wa Ngassa.
Hapo ndipo Kamati ya Sheria na Hadhi ya Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TTF) ikanasa. Kwa woga haikutaka kuiadhibu Yanga kwa faulo iliyofanya, na kwa woga haikutaka kutupilia mbali mkataba wa Simba.
Kamati hiyo ikaamua kupita njia salama. Imetambua mkataba wa Ngassa na Simba na imetambua pia mkataba wa Ngassa na Yanga, lakini kwa vile Msimbazi hawakukamilisha fomu za usajili, kamati ikamhalalisha kukipiga Jangwani ambako taratibu za usajili zilikamilishwa.
Hata hivyo, TFF imemtaka Ngassa kurejesha Sh. 30 milioni alizopewa kama kishika uchumba wa yeye kuichezea klabu hiyo msimu huu na Sh. 15 milioni kama fidia kwa Simba. Ameadhibiwa pia kutocheza mechi sita na hatacheza mpaka alipe fedha hizo.
Ngassa hana fedha hizo, na ilivyo Yanga imejiona imeadhibiwa, sasa inahaha kutaka mchezaji huyo asiadhibiwe. Yanga hata kama itakata rufani, katika sakata hili, kikanuni haihusiki.
Kwa kuwa TFF inatambua usajili wa mchezaji baada ya kukamilisha fomu mama za usajili zenye picha na saini, Simba inaweza kukataa haikumsajili Ngassa akiwa na usajili wa Azam.
Lakini hatua ya klabu hiyo kuingia naye mkataba 2 Agosti 2012 ni kosa kikanuni kwani huko ni kufanya mazungumzo kabla ya muda unaotakiwa.
Kwa mujibu wa Kanuni za Usajili wa wachezaji wa Ligi Kuu ya Vodacom, Simba ilipaswa kuadhibiwa kwa kosa la kuingia mkataba juu ya mkataba wa Ngassa na Azam.
Ibara ya 5 ya Kanuni za Fifa kuhusu Usajili na Hadhi ya Wachezaji sehemu ya 3 inasema kuwa “Mchezaji anaruhusiwa kuichezea klabu moja tu kwa wakati.”
Kanuni ya 37 kuhusu usajili sehemu ya 2 inasema “Mchezaji anaweza kusajiliwa na klabu moja kwa wakati huo na sio vinginevyo”.
Kanuni ya 44 kuhusu Masharti ya mikataba kati ya wachezaji na klabu sehemu ya 2 inasema klabu inayotarajia kuingia mkataba na mchezaji wa kulipwa haina budi kuiarifu klabu yake ya sasa kwa maandishi kabla ya kufanya makubaliano na mchezaji huyo wa kulipwa. Mchezaji wa kulipwa atakuwa huru tu kuingia mkataba na kilabu nyingine iwapo mkataba wake na kilabu yake ya sasa umekwisha au utakwisha baada ya miezi sita (6). Uvunjaji wowote wa sharti hili utastahili vikwazo vinavyofaa.
Makubaliano yaliyokuwepo kati ya Simba na Azam yalikuwa ya Ngassa kucheza kwa mkopo lakini kwa ujanjaujanja wakaingia mkataba usiohusika.
Vilevile, Ibara ya 42 ya Kanuni za Ligi Kuu ya Vodacom kuhusu Kuazimwa kwa mkopo kwa wachezaji wa kulipwa zinaeleza wazi.
(1)     Mchezaji wa kulipwa anaweza kuazimwa kwa mkopo na klabu nyingine kwa msingi wa makubaliano ya maandishi kati yake na klabu zinazohusika. Uazimwaji huo wa mkopo utafuata sheria zilezile zinazotumika katika uhamisho wa wachezaji, yakiwemo masharti ya       fidia ya mafunzo na utaratibu wa mshikamano.
(2)     Kufuatana na Ibara ya 5(3), ya kanuni za FIFA kipindi cha chini cha mchezaji kuazimwa kwa mkopo kitakuwa ni muda kati ya vipindi viwili vya usajili.
(3)     Klabu itakayompokea mchezaji kwa msingi wa kuazimwa kwa mkopo haina haki ya kumhamishia katika klabu nyingine bila ya idhini ya maandishi ya klabu iliyomwachia                      mchezaji kwa mkopo na ya mchezaji anayehusika.
Kanuni hizo zote zinaelezea kwa uwazi masharti ya usajili, lakini si mikataba. Kama mkataba wa Simba na Ngassa uliochapwa magazetini ni sahihi, Simba ikijua hakuna kifungu kinachowabana kuhusu mikataba ilimlazimisha Ngassa kutia saini mkataba wa nyongeza huku akiwa mchezaji halali wa Azam.
Kwa kuwa Simba na Yanga zimeona matundu katika kanuni za mikataba na usajili, TFF iangalie uwezekano wa kuboresha kanuni kuzibana klabu hizo zisiendelee kuumiza wachezaji.

Makala hii imetolewa kwenye gazeti la Mawio
Tagged
Different Themes
Written by Templateify

Aenean quis feugiat elit. Quisque ultricies sollicitudin ante ut venenatis. Nulla dapibus placerat faucibus. Aenean quis leo non neque ultrices scelerisque. Nullam nec vulputate velit. Etiam fermentum turpis at magna tristique interdum.

0 comments